1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UN:yapitisha azimio muhimu kuhusu Tabianchi

30 Machi 2023

Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa limepiga hatua kubwa baada ya wajumbe kupitisha azimio la kuitaka Mahakama ya Kimataifa ya Haki ICJ kuelezea wajibu wa kisheria wa mataifa kuhusiana na kupunguza ongezeko la joto duniani.

https://p.dw.com/p/4PTOL
USA New York | UN-Vollversammlung | Wassili Nebensja
Picha: Timothy A. Clary/AFP/Getty Images

Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa limepiga hatua kubwa baada ya wajumbe kupitisha azimio la kuitaka Mahakama ya Kimataifa ya Haki ICJ kuelezea wajibu wa kisheria wa mataifa kuhusiana na kupunguza ongezeko la joto duniani.

Shangwe zilisikika huku hatua hiyo ikitajwa kuwa ni ushindi kwa vuguvugu la haki ya mabadiliko ya Tabianchi ambalo linatazamiwa kuongeza shinikizo kwa nchi zinazochafua mazingira na kushindwa kushughulikia dharura ya ongezeko la joto duniani.

Likisukumwa kwa miaka mingi na vijana kutoka Jamhuri ya Vanuatu, kisiwa kidogo ambacho mustakabali wake unatishiwa na kupanda kwa kina cha bahari ya Pasifiki.

Azimio hilo lililofadhiliwa na zaidi ya nchi wanachama 130, ilitarajiwa kuidhinishwa na idadi kubwa ya nchi wanachama.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres  amesema hatua hiyo imeweka historia huku akisisitiza kwamba hata kama kutofungamana,kwa maoni ya kisheria ya Mahakama ya ICJ itasaidia Baraza Kuu, Umoja wa Mataifa na nchi wanachama kuchukua hatua pana na madhubuti.

Soma pia:UN kutoa ripoti ya kupambana na mabadiliko ya tabianchi

Amesema haki ya hali ya hewa ni sharti la kimaadili na sharti la hatua madhubuti ya hali ya hewa duniani.

"Mgogoro wa hali ya hewa unaweza tu kutatuliwa kwa ushirikiano" Alisema Guterres

Aliendelea kufafanua mbele ya wajumbe wa Baraza kuu "kuongezeka kwa ukosefu wa haki dhidi ya hali ya hewa kunasababisha migawanyiko na kutishia kulemaza hatua za mabadiliko ya Tabianchi.”

Je,mataifa yanamsukumo wa kisheria?

Ingawa mataifa hayana wajibu wa kisheria chini yaMkataba wa Paris wa 2015 kufikia malengo ya kupunguza uzalishaji, waungaji mkono wa azimio hilo jipya wanatumia mwanya mwingine, ikiwa ni pamoja na Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Sheria ya Bahari, unaoweza kutoa njia za utekelezaji.

Karte Inselstaaten im Südwest-Pazifik DE
Ramani ikionesha nchi za Kusini Magharibi mwa Bahari ya Pasifiki:Chanzo DW

Waziri Mkuu wa Vanuatu Alatoi Ishmael Kalsakau ambae nchi yake ilikuwakinara katika kufikia lengo la kupitishwa azimio hilo ameliambia Baraza kuu la Umoja wa Mataifa kwamba,haya si mafanikio makubwa mno ya kujivunia.

Soma pia:Ujerumani na India kushirikiana kulinda mazingira

Amesema, mafanikio hayo yanamchango mkubwa katika mabadiliko ya Tabianch,maamuzi ya hali ya hewa,ikiwa ni pamoja na kuchochea nia ya dhati chini ya mkataba wa Paris.

"Kutoa haki ya hali ya hewa umuhimu unaostahili, na kuleta ukamilifu wa sheria za kimataifa kukabiliana na changamoto hii ambayo haijapata kifani. Tunaamini kuwa ICJ inaweza kufanya hivi."

Sehemu ya hotuba yake mbele ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ilisema kabla ya kupitishwa kwa azimio hilo.

Jicho la wataalamu wa sheria za kimataifa kwenye azimio

Ingawaje maoni ya mahakama ya ICJ hayafungamani,hata hivyo yanabeba uzito mkubwa wa kisheria na kimaadili na mara nyingi huzingatiwa na mahakama za kitaifa.

Benoit Mayer, mtaalamu wa sheria za kimataifa katika Chuo Kikuu cha China cha Hong Kong,akizungumza na shirika la habari la AFP ameonya uwezekano wa janga la kimazingira iwapo maoni ya ICJ yakienda kinyume na kile wafuasi wa ombi hilo walitaka.

Azimio hilo linaitaka ICJ kufafanua hasa "matokeo ya kisheria" kwa mataifa ambayo "yamesababisha madhara makubwa kwa mfumo wa hali ya hewa na sehemu nyingine za mazingira.

Soma pia:COP27: Nishati mbadala kusaidia hali ya hewa, usalama

Linaenda mbali na kuitaka mahakama kupima wajibu kwa "nchi ndogo za visiwa zinazoendelea," ambazo zipo kwenye "hatari zaidi" kwa mabadiliko ya hali ya hewa, pamoja na wajibu kwa vizazi vijavyo.

Azimio hilo la kihistoria linapitishwa wakati ambapo, ripoti ya hivi karibuni kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi ikionya kwamba ili kupunguza ongezeko la joto duniani hadi nyuzi joto 1.5 Celsius,uzalishwaji wa hewa chafu lazima upunguzwe karibu nusu hadi kufikia 2030.

Mabadiliko ya tabianchi yameathiri vipi maisha yako?