1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUkraine

Blinken: Msaada wa kijeshi kwa Ukraine utawasili karibuni

14 Mei 2024

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken amewasili mjini Kyiv leo ili kuihakikishia Ukraine inao uungwaji mkono wa Washington,wakati huu ambao inaendelea kujilinda dhidi ya mashambulizi yanayoongezeka ya Urusi.

https://p.dw.com/p/4fps7
Kyiv, Ukraine | Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky
Wais wa Ukraine Volodymyr Zelensky akimlaki mgeni wake Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken, mjini Kyiv.Picha: Ukrainian Presidential Press Office/AP/picture alliance

Ziara hiyo ya Blinken inafanyika ikiwa ni chini ya mwezi mmoja baada ya Bunge la Marekani Congress kuidhinisha msaada wa kijeshi wenye thamani ya dola bilioni 60 kwa Ukraine baada ya kukwama kwa muda mrefu huku kukiwa na vuta n'kuvute miongoni mwa wabunge.

Akilakiwa na mwenyeji wake Rais wa Ukraine Volodymir Zelensky, Blinken amesema Washington inatambua kuwa vikosi vya Ukraine vinapitia wakati mgumu kwenye uwanja wa mapamabano.

Blinken amemuhakikishia rais Zelensky kwamba msaada kutoka kwenye kifurushi kipya utawasili hivi karibuni ambao ana matumaini kuwa "utaleta mabadiliko ya kweli" katika uwanja wa vita, katika wakati huu vikosi vya Urusi vikiendelea kutwaa udhibiti katika baadhi ya maeneo, dhidi ya vikosi vya Ukraine ambavyo vimekuwa vikikabiliwa na changamoto chungumzima ikiwamo uhaba wa silaha.

Soma pia:Ujerumani na nchi za Nordic zaahidi kuendelea kuiunga mkono Ukraine

"Awamu hii mpya ya msaada upo njiani kuwasili na mingine mingi itafuata," alisema Blinke kwenye mazungumzo yake na Rais Zelensky.

"Ninauhakika kifurushi hiki cha msaada kitaleta tofauti kubwa dhidi ya uvamizi wa urusi na hata kwenye uwanja wa vita." Aliongeza.

Tangu Rais wa Marekani Joe Biden atie saini kifurushi cha msaada uliocheleweshwa kwa Ukraine mwezi uliopita utawala tayari umetangaza kiasi cha dola bilioni 1.4 kama msaada wa kijeshi wa muda mfupi na dola bilioni 6 kwa msaada wa muda mrefu.

Washington itafikisha msaada huo kwa wakati?

Mshauri wa masuala ya usalama wa Marekani Jake Sullivan hapo jana Jumatatu alisema kwamba Washington inajaribu kuharakisha usafirishaji wa silaha kwenda Ukraine.

Kyiv, Ukraine I Ujumbe wa Marekani na Ukraen wakiwa kwenye mazungumzo
Ujumbe wa kidiplomasia wa Marekani ukiwa kwenye mazungumzo na ujumbe wa Ukraine wakati wa ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony BlinkenPicha: Brendan Smialowski/AP/picture alliance

Aidha rais Zelensky ameishukuru Washington kwa msaada huo akisema kwamba "uidhinishwaji wa kifurushi cha msaada kwa Ukraine ilikuwa ni muhimu kwao."

Zelensky alimwambia mwanadiplomasia huyo wa Marekani kwamba, uhaba mkubwa kwa vikosi vyake ni mifumo ya ulinzi wa anga huku akiomba pia betri mbili za makombora aina ya Patriot katika mkoa wa Kharkiv mbapo vikosi vya Urusi vimekuwa vikisonga mbele na kuvishambulia vijiji vya mpakani.

Soma pia:Ukraine yasema imedungua droni 59 na makombora ya Urusi

Hadi sasa Washington inasema tayari baadhi ya msaada umekwisha wasilishwa nchini Ukraine ikiwemo mifumo ya ulinzi wa anga, makombora ya masafa marefu.

Hii ni ziara ya nne ya Blinken mjini Kyiv tangu Urusiilipofanya uvamizi kamili nchini Ukraine mnamo Februari 2022, katika ziara yake hii anatarajiwa pia kuzungumza na mashirika ya kiraia katika kile maafisa wa Marekani wanasema ni kutathmini athari za vita na kujadili mustakabali wa uchumi wa Ukraine.

Wanajeshi wa Urusi waondoka Kharkiv

Katika uwanja wa vita, jeshi la Ukraine limesema hali katika mkoa waKharkiv imerejea kwenye utulivu kufuatia mashambulizi makali, licha ya ukweli kwamba huenda vikosi vya Urusi vikaanzisha tena mashambulizi katika siku za usoni.

Soma pia:Hujuma za Urusi zaendelea kuutikisa mji wa Kharkiv, Ukraine

Mapema leo jeshi hilo limesema vikosi vya Urusi pia vimeondoa wapiganaji wake kwenye mji wa Vovchansk huko Kharkiv na kuongeza kwamba idadi ya mashambulizi kwenye eneo hilo imepungua kwa kiwango kikubwa.

Ujerumani: Hatutaiacha Ukraine kwenye vita peke yake

Wakati hayo yakiendelea Rais wa Urusi Vladimry Putin anatarajiwa kukutana na mshirika wake wa karibu rais Xi Jinping wa China akisaka kile kinachotajwa uungwaji mkono wa Beijing kwenye vita vyake vinavyoendelea nchini Ukraine.