1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yapiga kura ya turufu juu ya uanachama wa Palestina

19 Aprili 2024

Azimio la kuungwa mkono uanachama kamili wa taifa la Palestina ndani ya Umoja wa Mataifa limeshindwa kupitishwa kwenye Baraza la Usalama la Umoja huo kufuatia kura ya turufu iliopigwa na Marekani.

https://p.dw.com/p/4ewpV
New York | Umoja wa Mataifa Balozi wa Marekani Robert Wood
Balozi wa Marekani Umoja wa Mataifa Robert Wood akizungumza mbele ya Baraza la Usalama mjini New York.Picha: Yuki Iwamura/AP/picture alliance

Nchi 12 zilipiga kura ya kuunga mkono azimio hilo huku Uswisi na Uingereza zikijuzuia.

Kura ya turufu ya Marekani, ambayo ni mwanachama wa kudumu wa chombo hicho chenye nguvu zaidi ndani ya Umoja wa Mataifa, ilimaanisha kuwa rasimu ya azimio hilo ilishindwa kupitishwa.

Ili kufanikiwa kwa azimio hilo linahitaji kupigiwa kura  na wanachama 9 kati ya 15 wa Baraza la Usalama na kuwepo na kura ya turufu kutoka kwa mwananchama yeyote kati ya watano wa kudumu wa Baraza hilo - China, Ufaransa, Urusi, Uingereza na Marekani.

Mamlaka ya Ndani ya Palestina imeulaani uamuzi huo wa Marekani na kuutaja kuwa ni "uchokozi" unaoisukuma mashariki ya Kati kuelekea shimoni.

Soma pia:Baraza la Haki la UN lataka Israel kuwajibishwa kwa uhalifu wa kivita huko Gaza

Mapema mwezi Aprili, Balozi wa Palestina wa Umoja wa Mataifa, Riyad Mansour, alimwandikia barua Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, akiomba hoja hiyo, ambayo tayari iliwasilishwa mwaka 2011, lakini haikuweza kupitishwa, iwasilishwe tena kwa Baraza la Usalama.

Israel yaapa kujibu mashambulizi ya Iran

Israel imeapa kujibu mashambulizi ya Iran ya mwishoni mwa juma ambayo yamesababisha hofu ya kutanuka kwa mzozo, baada ya miezi kadhaa ya mapigano yaliosababisha maelfu ya watu kuuwawa na wengine kujeruhiwa katika eneo la Ukanda wa Gaza.

Umoja wa Mataifa- Baraza la Usalama | Balozi wa Israel Umoja wa Mataifa Gilad Erdann
Balozi wa Israel Umoja wa Mataifa Gilad Erdann akionesha picha mbele ya Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa namna Iran ilivyoendesha mashambulizi yake.Picha: Yuki Iwamura/Anadolu/picture alliance

Washirika wa Israel wamekuwa wakiitaka kujizuia kufuatia shambulio hilo la Iran ambayo kwa sasa viongozi wa Umoja wa Ulaya wameapa kuongeza mbinyo wa vikwazo dhidi yake wakilenga usafirishaji wake wa ndege zisizo na rubani na makombora kwa washirika wake wa Ukanda wa Gaza, Yemen na Lebanon.

Marekani ambayo nayo iliweka vikwazo ambavyo vimelenga watu binafsi pamoja na wazalishaji wa zana hizo. mashambulizi ya Iran siku ya Jumamosi, yaliashiria mara ya kwanza kwa Tehran kufanya shambulio la kijeshi na la moja kwa moja dhidi ya Israel.

Mamlaka ya Israel ilisema Iran ilirusha zaidi ya makombora na droni 300 na asilimia 99 ya mashambulizi hayo yalizuiliwa na mifumo ya ulinzi wa anga wakishirikiana na Marekani, Uingereza, Ufaransa na Jordan.

Soma pia:Kwanini Iran na Israel ni maadui?

Iran imesema siku ya Ijumaa kuwa imedungua ndege kadhaa zisizo na rubani na kwamba "hakujakuwa na shambulio la kombora kwa sasa" nchini humo, baada ya milipuko kusikika karibu na mji wa kati wa Isfahan.

Ndege kadhaa zisizo na rubani "zikudunguliwa na kikosi cha anga, hakuna ripoti za shambulio la kombora kwa sasa," msemaji wa shirika la anga la Iran Hossein Dalirian aliandika katika mtandao wa X.

Hapo awali shirika la habari la Fars lilisema "milipuko mitatu" ilisikika karibu na kambi ya jeshi la jeshi la Shekari karibu na mji wa Isfahan.

Iran inaweza kumudu vita na Israel?