1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUfaransa

Wakulima waandamana nchini Ufaransa

Saumu Mwasimba
29 Januari 2024

Wakulima wanaoandama Ufaransa wameapa kuufunga mji mkuu Paris kwa matrekta leo Jumatatu kuishinikiza serikali isikilize kilio chao kuhusu hatma ya sekta hiyo ya kilimo nchini Ufaransa.

https://p.dw.com/p/4bnmn
Wakulima wa Ufaransa wakiandamana
Wakulima wa Ufaransa wakiandamanaPicha: Moritz Thibaud/ABACA/IMAGO

Wakulima wanalalamika kwamba sekta hiyo imepata mtikisiko mkubwa kutokana na vita vya Ukraine.

Misururu ya magari ya wakulima imeonekana kuzifunga barabara kuu za kuelekea mji wa Paris huku maandamano pia yakishuhudiwa katika maeneo mengine ya nchi hiyo katika kile kinachoonekana kuwa wiki nyingine ngumu kwa waziri mkuu mpya Gabriel Attal, aliyeingia madarakani chini ya mwezi mmoja.

Wakulima wa Ufaransa wanalalamikia kupanda kwa bei za mbolea, nishati na pembejeo nyingine za kilimo zinazotumika kuzalisha mazao na kulisha mifugo,hali iliyofanya kilimo kuwa kigumu kwa baadhi ya wakulima.

Pia wanalalamika kwamba hawana ruzuku ya kutosha na wanabanwa na sheria nyingi zilizowekwa za kuhifadhi mazingira.Maandamano ya wakulima yameshuhudiwa pia katika nchi nyingine za Ulaya kama Ujerumani, Ubelgiji, Lithuania, Uholanzi, Poland na Romania.