1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wakenya waomboleza kifo cha mkuu wa majeshi

Saumu Mwasimba
19 Aprili 2024

Kenya imeanza siku tatu za maombolezo baada ya mkuu wake wa majeshi na maafisa tisa waandamizi jeshini kufariki dunia kufuatia ajali ya helikopta iliyotokea siku ya Alhamisi (Aprili 18).

https://p.dw.com/p/4exzn
Aliyekuwa mkuu wa jeshi la Kenya, Meja Jenerali Francis Omondi Ogolla.
Aliyekuwa mkuu wa jeshi la Kenya, Meja Jenerali Francis Omondi Ogolla.Picha: LUIS TATO/AFP/Getty Images

Jenerali Francis Omondi Ogolla, mkuu wa jeshi la ulinzi la Kenya, na maafisa wake walikufa baada ya helikopta iliyokuwa imewabeba kuanguka muda mfupi baada ya kuruka kaskazini magharibi mwa nchi hiyo.

Akitangaza msiba huo jioni ya Alhamisi, Rais William Ruto alisema majenerali hao walipoteza maisha wakiwa kazini kuitumikia nchi yao na bendera zingelipepea nusu mlingoni ndani hadi kwenye balozi zake zote nje ya nchi.

Soma zaidi: Mkuu wa majeshi Kenya afariki katika ajali ya ndege

Miili ya majenerali hao ilipelekwa katika kambi ya jeshi mjini Nairobi usiku wa kuamkia Ijumaa.

Ogolla aliteuliwa mkuu wa majeshi na RTais Ruto mwaka uliopita na alikuwa anakaribia kutimiza miaka 40 tangu kujiunga jeshini.

Ripoti za vyombo vya habari nchini Kenya zinasema ni ajali ya tano inayohusisha helikopta za jeshi katika kipindi cha miezi 12 huku ikidaiwa kwamba ndege za jeshi nchini humo zimechakaa na hazina huduma nzuri wala matengenezo.