1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaBrazil

Viongozi walaani uvamizi wa majengo ya serikali Brazil

9 Januari 2023

Mamlaka nchini Brazil leo zimeanza uchunguzi kufuatia uvamizi wa majengo ya serikali uliofanywa na maelfu ya wafuasi wa rais wa zamani wa nchi hiyo Jair Bolsonaro.

https://p.dw.com/p/4LtlH
Brasilien Brasilia | Bolsonaro Anhänger im Palácio do Planalto
Picha: Eraldo Peres/AP Photo/picture alliance

Waandamanaji hao waliokuwa wamevalia mavazi yenye rangi ya bendera ya nchi hiyo hapo jana, walilivamia bunge, mahakama ya juu na kasri la rais ambapo walivunja vioo, samani, kompyuta na vifaa vingine.

Waziri wa sheria wa Brazil Flavio Dino amesema matukio hayo ni sawa na ugaidi na kuchochea mapinduzi na kwamba mamlaka zimeanza kuchunguza waliolipia mabasi ya kuwasafirisha waandamanaji kuelekea mji mkuu.

Polisi ya Brazil imesema watu 300 tayari wameshakamatwa. Viongozi mbalimbali duniani wamelaani tukio hilo.

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz amesema uvamizi huo ni sawa na uvamizi wa demokrasia na hauwezi kukubalika. Waziri Mkuu wa Uingereza Rishi Sunak naye amesema Uingereza iko pamoja na Brazil na rais wake mpya Lula Da Silva.