1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUjerumani

Ujerumani yamwita balozi wa Iran kufuatia shambulizi Israel

Amina Mjahid
15 Aprili 2024

Msemaji wa wizara ya mambo ya nchi za nje ya Ujerumani amesema nchi hiyo imemuita balozi wa Iran, kufuatia mashambulizi yaliyofanywa na Tehran dhidi ya Tel Aviv siku ya Jumamosi.

https://p.dw.com/p/4eoIn
ARCHIV | Iran | Militärübung mit iranischen Drohnen
Picha: Iranian Army Office/ZUMA Wire/IMAGO

Iran imesema hatua iliyochukuliwa inaonesha misimamo isiyowajibika ya Ujerumani, Ufaransa na Uingereza ambazo zote zimewaita mabalozi wa Iran katika nchi zao kujadili shambulio hilo.

Italia nayo inayoshikilia urais wa kupokezana wa kundi la nchi tajiri kiviwanda la G7 imesema kupitia waziri wake wa mambo ya nje Antonio Tajani,  kwamba iko tayari kwa hatua ya kuwawekea vikwazo watu binafsi watakaohusika na mashambulizi dhidi ya Israel.

Kwa mara ya kwanza katika historia, Iran imeishambulia moja kwa moja adui yake wa miaka mingi Israel kwa  droni zaidi ya 300 pamoja na kuifyetulia  makombora yaliyofanikiwa kudunguliwa kwa asilimia 99.

Iran ilikuwa inajibu shambulizi linalodaiwa kufanywa na Israel katika ubalozi wake mdogo nchini Syria lililosababisha mauaji ya makamanda wake.