1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Steinmeier: Sote tunatamani ulimwengu wa amani zaidi

Iddi Ssessanga
25 Desemba 2023

Katika hotuba yake ya Krismasi, Rais wa Shirikisho Frank-Walter Steinmeier amewasihi Wajerumani wasiache kutamani ulimwengu wenye amani zaidi, akisema kuna “washauri bora zaidi kwa watu kuliko hasira na dharau.

https://p.dw.com/p/4aYHN
Ujerumani| Hotuba ya Krismas ya Rais wa Shirikisho Steinmeier
Frank-Walter Steinmeier anahimiza umoja, akisema watu wanaofanya kazi pamoja wanaweza kuifanya nchi kuwa na nguvu zaidi.Picha: Britta Pedersen/dpa-Pol/picture alliance

Rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier amezungumzia haja ya ujasiri na ushirikiano katika kukabiliana na changamoto nchini Ujerumani na duniani kote katika hotuba yake ya kila mwaka ya Krismasi.

"Mwaka huu, kwa hakika ulimwengu umedhihirisha upande wake wa giza," Steinmeier alisema, kulingana na maandishi ya hotuba yake iliyotolewa na ofisi yake kabla ya kurushwa na vituo vya utangazaji Siku ya Krismasi.

"Vita vya uchokozi vya Urusi dhidi ya Ukraine sasa vinaingia katika msimu wake wa baridi wa pili," Steinmeier alisema. "Na, tangu msimu wa vuli, tumekuwa tukitazama kwa mshtuko ukatili wa Hamas na kile kinachotokea kwa wahanga wa vita katika Mashariki ya Kati."

Soma pia: Hotuba ya Krismasi: Rais wa Ujerumani atoa wito wa kuzingatiwa 'amani na haki' nchini Ukraine.

Licha ya changamoto hizo, Steinmeier alisisitiza umuhimu wa matumaini na haja ya kuukaribia mwaka mpya kwa ujasiri na azma.

Ujerumani| Hotuba ya Krismas ya Rais wa Shirikisho Steinmeier
Rais wa shirikisho la Ujerumani Frank-Walter Steinmeier amesema dunia imeonyesha 'upande wake wa giza' mwaka huu.Picha: Britta Pedersen/dpa-Pol/picture alliance

"Sote tunatamani ulimwengu wenye amani zaidi," alisema, akisisitiza imani yake kwamba "tunapaswa kamwe kuachana" na hii.

Steinmeier: 'Fanyeni kazi pamoja'

Rais huyo wa Ujerumani alisisitiza umuhimu wa kudumisha demokrasia imara, akisema kwamba hilo linaweza kutokea tu ikiwa watu watashirikishwa na ikiwa watajitahidi "kuhakikisha kwamba kile ambacho bado hakijawa kizuri leo kinakuwa bora kesho."

Steinmeier alikiri kwamba mwaka huu umewaacha Wajerumani wengi wakiwa na wasiwasi kuhusu "maswala ambayo hayajatatuliwa hapa nchini kwetu" bila kuyataja moja kwa moja.

Baadhi ya Wajerumani wameonyesha mashaka juu ya uwezo wa serikali kutatua changamoto hizo, huku wengine wakielezea wasiwasi wao kuhusu athari za muda mrefu za masuala haya.

"Tutaweza kuoiga hatua tu ikiwa tutafanya kazi pamoja - na sio ikiwa kila mtu atarudi kwenye ulimwengu wake," Steinmeier alisema.

Matarajio ya sherehe

Hotuba hiyo ilijumuisha shukrani kwa polisi, wazima moto, wanajeshi, wafanyikazi wa afya na taasisi nyingine.

"Kuna mamilioni ya watu kama nyinyi, wamedhamiria na kujitolea katika kuwasaidia wengine, wanaofanya kazi kwa ajili ya kuishi pamoja kwa amani katika jamii tofauti," Steinmeier alisema. "Na ni watu hawa wanaonipa ujasiri."

Somapia: Steinmeier achaguliwa rais wa Ujerumani kwa muhula wa pili

Akizungumzia matarajio yake kwa mwaka ujao, Steinmeier alibainisha kuwa Sheria ya Msingi ya Ujerumani inatimiza miaka 75 na inapaswa kusherehekewa.

"Katiba yetu ni kitu ambacho tunaweza kujivunia," Steinmeier alisema. "Inalinda na kuthamini kila mtu."

Ujerumani yaiomba Tanzania radhi kwa madhila ya Ukoloni

Steinmeier alisema katiba hiyo inaweza kuliongoza taifa katika nyakati zenye changamoto.

"Hebu tuchukue muda kila mara kukumbuka kuwa Ujerumani ni, na inasalia kuwa nchi nzuri," Steinmeier alisema.

"Tunaweza na tutafaulu ikiwa tutafanya juhudi, ikiwa tutasimama pamoja na kukaa pamoja," rais alisema.