1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani 'kuipiga jeki' Ghana

Mohammed Khelef
28 Machi 2023

Makamu Rais wa Marekani Kamala Harris ameahidi kwamba nchi yake itaisaidia Ghana ambayo inakabiliwa na mgogoro wa kiuchumi na wasiwasi wa kiusalama.

https://p.dw.com/p/4PMmu
Ghana | Kamala Harris in Accra
Picha: MISPER APAWU//AFP/Getty Images

Makamu huyo wa rais wa Marekani alizungumza hayo mjini Accra, kituo cha kwanza cha ziara yake barani Afrika, ambako alikutana na rais wa nchi hiyo, Nana Akufo Addo. 

Katika mkutano na waandishi habari  pamoja na Rais Addo, Kamala Harris alisema chini ya uongozi wa Rais Addo, "Ghana imekuwa mwanga wa demokrasia na mchangiaji wa amani na usalama duniani."

Soma: Makamu wa rais wa Marekani aanza ziara yake katika nchi tatu barani Afrika ambapo yuko nchini Ghana

Alitangaza msaada wa dola milioni 100 na kuahidi kwamba Marekani itaimarisha ushirikiano wake na bara zima la Afrika.

Aidha serikali ya Marekani imeliomba bunge dola milioni 139 nyingine kwa ajili ya kuisadia Ghana kupunguza kiwango cha watoto wanaofanyishwa kazi, kuimarisha shughuli za utafiti wa hali ya hewa, kuwasaidia wanamuziki nchini humo pamoja na kukabiliana na miripuko ya magonjwa.