1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kenya yatimiza mwaka mmoja tangu mauaji ya Shakahola

Saumu Mwasimba
19 Aprili 2024

Kenya wiki hii inafanya kumbukumbu ya mwaka mmoja tangu yalipogunduliwa makaburi yaliyozikwa mamia ya watu waliokufa kutokana na njaa baada ya kujizuia kula na kunywa kwa muda mrefu kufuatia imani ya kiroho yenye utata.

https://p.dw.com/p/4exyE
Afrika Mombasa Paul Mackenzie
Mchungaji Paul Mackenzie akiwa mahakamani mjini Mombasa.Picha: Halima Gongo/DW

Mkasa huo uliopewa jina la "Mauaji ya Shakahola" ulisababisha mshtuko dunia nzima. 

Vifo hivyo inadaiwa vilisababishwa na mtu anayejiita kiongozi wa kiroho, Paul Nthenge MacKenzie, ambaye anatuhumiwa kuwachoea waumini wake kuishi bila ya kula wala kunywa chochote hadi wafe ili wapate fursa ya kile anachosema ni ''kukutana na Yesu.''

Awamu nyingine ya ufukuaji miili msitu wa Shakahola -Kenya

Inadaiwa kwamba kiongozi huyo aliweka genge maalum la kuwasimamia waumini kuhakikisha hakuna anayekwenda kinyume na ibada hiyo ya kufunga au anayeondoka akiwa hai kwenye eneo hilo la msitu yalikokuweko makaazi ya kanisa lake. 

Miili 429 imeshapatikana hadi sasa baada ya kufukuliwa makaburi kadhaa kwenye msitu huo huku duru nyingine ya kufukua makaburi ikiwa imepangwa kuendelea mwaka huu.