1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Joto kali kwenye eneo la Arctic laongeza kitisho ulimwenguni

Lilian Mtono
14 Desemba 2021

Shirika la kimataifa la hali ya hewa limetambua kiwango kipya cha juu zaidi cha joto ulimwenguni katika eneo la Arctic, hali inaobua kitisho kikubwa cha mabadiliko ya hali ya hewa ulimwenguni.

https://p.dw.com/p/44EQZ
UK | Schneehase in Schottland
Picha: Frischknecht Patrick/prisma/picture alliance

Kulingana na shirika hilo, kiwango hicho cha juu kabisa cha joto cha nyuzijoto 38 za Celcius kilirekodiwa mwaka jana nchini Serbia, ikiwa ni mfululizo wa msururu wa viwango vya juu vya joto vinavyoibua wasiwasi mkubwa ulimwenguni. 

Mkuu wa shirika hilo la hali ya hewa na Umoja wa Mataifa, WMO Petteri Taalas amesema kwenye taarifa hiyo kwamba viwango hivyo vya juu kabisa vinavyoshuhudiwa sasa vinaashiria kitisho kinachoukabili ulimwengu kuhusiana na mabadiliko ya tabianchi.

Joto kali ambalo ni sawa na nyuzijoto 100.4 Fahrenheit liliorodheshwa Juni 20 mwaka jana katika mji wa Verkhoyansk nchini Urusi na kuwa kiwango cha juu kabisa kuwahi kufikiwa katika uzingo wa Arctic kulingana na shirika hilo.

Soma Zaidi: COP26: Viongozi wa dunia kujadiliana kukabili ongezeko la joto

Hii ni mara ya kwanza kwa WMO kuongeza taarifa za viwango vilivyopindukia vya joto katika eneo la Arctic katika idara yake ya kumbukumbu za hali mbaya ya hewa na ripoti hii imechapishwa wakati kukishuhudiwa wimbi lisilotabirika la viwango vilivyopindukia vya joto kote ulimwenguni.

Mji wa Verkhoyansk uko kilomita 115 kaskazini mwa Uzingo wa Arctic na viwango vyake vya joto vimekuwa vikifuatiliwa tangu mwaka 1885.

Narwhal
Joto kali katika eneo la Arctic pia lilichochea kuyeyuka kwa barafu bahariniPicha: Rights Managed/imago images/Ardea

Wastani wa joto katika eneo lote la Siberia lililoko Arctic wakati wa majira ya joto ya mwaka jana ulipindukia nyuzijoto 10 na hali hiyo ilisababisha  joto kali lililochochea upotevu mkubwa wa barafu baharini.

Mkuu huyo wa WMO aidha amesema, mawimbi la joto yalichangia pakubwa mwaka 2020 kuwa miongoni mwa miaka mitatu iliyokuwa na joto kali zaidi ulimwenguni. Katika kipindi hicho pia kulishuhudiwa kiwango cha juu kabisa cha nyuzijoto 18.3 katika bara la Antactic.

Lakini kwa upande mwingine shirika hilo limesema bado linahitaji kuthibitisha kiwango cha nyuzijoto 54.4 kilichorekodiwa mwaka 2020 na 2021 katika eneo lenye joto kali zaidi ulimwenguni la Death Valley katika jimbo la California nchini Marekani. Wataalamu wake pia wako mbioni kuthibitisha rekodi mpya ya joto ya nyuzijoto 48.8 iliyoripotiwa katika kisiwa cha Sicily nchini Italia katika majira ya joto ya mwaka jana.

Idara hiyo ya kumbukumbu ya shirika la WMO hufuatilia viwango vya juu kabisa na vya chini vya mvua, joto, ukame wa muda mrefu, kiwango cha juu cha upepo, radi za muda mrefu na vifo vinavyohusiana na majanga ya hali ya hewa.

Kuongezwa kwa rekodi hii mpya ya joto katika eneo la Arctic kunaashiria mabadiliko makubwa ya hali ya hewa. Ingawa maeneo yote ya ulimwengu yanakabiliwa na ongezeko la joto, baadhi yanaathirika haraka zaidi ya mengine, na kasi ya athari kwa Arctic ni zaidi ya mara mbili ya wastani wa kimataifa.

tazama Picha: 

Mashirika: AFPE