1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Borussia Dortmund imeifunga Paris Saint German 1-0

Sudi Mnette
2 Mei 2024

Mkondo wa kwanza wa nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa barani Ulaya kati ya Borussia Dortmund ya Ujerumani dhidi ya mabingwa wa Ligi Kuu nchini Ufaransa Paris Saint German PSG umalizika kwa Dortmund kuichapa PSG 1-0

https://p.dw.com/p/4fPSS
Nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa | Dortmund - PSG
Ligi ya Mabingwa, Borussia Dortmund ilipokutana na Paris Saint-Germain, Signal Iduna Park, Dortmund.Picha: Horst Mauelshagen/pepphoto/picture alliance

Ulikuwa mchuano mkali na aina yake ambapo tathmini zilionesha Paris Saint-Germain, kuutawala mchezo dhidi ya Borussia Dortmund ingawa yote, kwa yote mpira magoli. Dakika tisini zilipokamilika ikawa ni Dortmund moja PSG sifuri.

Mshambulizi wa Borussia Dortmund Niclas Füllkrug kwa wakati wote ndie aliganda katika vichwa vya mashabiki wa Borussia Dortmund baada ya kuipa bao pekee la ushindi timu yake kunakodakikaya 36 katika kipindi cha kwanza. Ikumbukwe tu huu ni mkondo wa kwanza wa mchuano wa nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa barani Ulaya kati ya timu hizi mbili.

Matunda ya pasi nzuri ya Schlotterbeck

Halbfinale der Champions League | Dortmund - PSG
Mchezaji wa Borussia Dortmund Niclas Fullkrug alipoifunga bao lake la kwanza akimpita Gianluigi Donnarumma wa Paris St GermainPicha: Thilo Schmuelgen/REUTERS

Mlinzi  wa Dortmund Nico Schlotterbeck alitoa pasi ndefu kwa Füllkrug, ambae nae aliidhibiti kwa mguso wake wa kwanza na kumtungua kipa wa PSG Gianluigi Donnarumma na hivyo kwa dakika hiyo ya 36 ya mchezo mashabiki wa Borussia Dortmund, ikawa kwao nderemo na vifijo katika uwanja wa nyumbani wa Signal Iduna.

Ushindi huu unaelezwa kuipa Dortmund kile kinachoonekana nafasi finyu kabla ya timu hiyo kucheza tena Jumanne ijayo na hasimu wake huyo kwa duru ya pili mjini Paris.

Katika ngwe ya mchuano huo, beki wa kati wa ParisSaint-GermainLucas Hernández ilibidi atoke nje ya uwanja baada ya kupata jeraha wakati wa nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa ya timu yake ya duru ya kwanza dhidi ya Borussia Dortmund.

Je majeruhi Lucas Hernández atarejea mapema uwanjani?

Nafasi ya Hernández alijazwa na Lucas Beraldo ikiwa dakika ya 42 kwa kile kilichoonekana kuwa kujeruhiwa mguu wa kushoto. Beki huyo alikuwa akijaribu kumuzuia mshambuliaji wa Dortmund, Niclas Füllkrug baada ya kufunga bao la kwanza kunako dakika ya 36.

PSG kama wanavyofahamika kwa kifupi, walifanya bidii zaidi mwanzoni mwa kipindi cha pili, wakati Kylian Mbappé alipopiga mkwaju uliogonga besela upande wa kulia na Achraf Hakimi akagonga nguzo ya kushoto.

Gregor Kobel aliokoa juhudi zilizofuata za Mbappé na Dortmund wakanusurika kibano.

Soma zaidi:Dortmund na PSG zatinga nusu fainali Ligi ya Mabingwa Ulaya

Washindi wa mechi hiyo ya mikondo miwili watacheza na Real Madrid au Bayern Munich katika fainali itakayopigwa huko London Juni Mosi. Wapinzani hao wa zamani walitoka sare ya 2-2 katika mechi yao ya duru ya kwanza ya nusu fainali ya kwanza mjini Munich siku ya Jumanne.