1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

IOC: Ulaya kuikosoa Urusi kurejea michezoni kunasikitisha

Bruce Amani
30 Machi 2023

Rais wa Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki IOC Thomas Bach amesema inasikitisha kuona baadhi ya serikali za Ulaya zinakosoa mpango wa kuwarejesha kikamilifu wanamichezo wa Urusi na Belarus katika mashindano ya kimataifa.

https://p.dw.com/p/4PW8i
IOC debattiert mögliche Wiederzulassung Russlands
Picha: FABRICE COFFRINI/AFP/Getty Images

IOC jana ilitoa orodha ya mapendekezo kwa mashirikisho ya kimataifa ya michezo ambayo yatawaruhusu wanamichezo wa Urusi na Belarus kurejea tangu walipofungiwa  mwaka jana kufuatia uvamizi wa Moscow nchini Ukraine.

Hata hivyo uamuzi huo haujumuishi Michezo ya Olimpiki ya Paris mwaka 2024. Uamuzi tofauti utafanywa baadae kuhusu hilo.

Lakini serikali za Ukraine, Poland na Jamhuri ya Czech miongoni mwa nyingine zimekasirishwa na mpango wa IOC wa kurejea kwa wanamichezo wa Urusi na Belarus, zikisema hawana nafasi katika ulimwengu wa michezo wakazi vita bado vinaendelea.

Bach amesema inasikitisha kuwa baadhi ya serikali hazitaki kuheshimu walio wengi ndani ya Jumuiya ya Olimpiki na wadau wote, wala uhuru wa michezo.