1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mfalme Charles III aonya usalama wa Ulaya uko hatarini

Bruce Amani
30 Machi 2023

Mfalme Charles III wa Uingereza ameviita vita vya Urusi nchini Ukraine kuwa ni kitisho kwa maadili ya kidemokrasia barani Ulaya.

https://p.dw.com/p/4PWGX
König Charles Rede Bundestag
Picha: Wolfgang Kumm/dpa/picture alliance


Katika hotuba ya kwanza kuwahi kufanywa na mfalme katika bunge la Ujerumani, Charles hata hivyo amesema washirika kama vile Ujerumani na Uingereza wanaweza kupata ujasiri kutokana na umoja wao.

Akizungumza zaidi kwa Kijerumani katika hotuba yake ya dakika 30, Charles amesema uamuzi wa Ujerumani kutuma msaada huo muhimu wa kijeshi kwa Ukraine ni wa kijasiri na wa kuthaminiwa.

Charles yuko kwenye ziara yake ya kwanza ya kigeni tangu alipokalia kiti cha Ufalme kufuatia kifo cha mama yake Malkia Elizabeth II mwaka jana, na chaguo lake la kwenda Ujerumani limeonekana kuwa jitihada ya kujenga uhusiano na Ulaya baada ya Brexit.