1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kiungo wa zamani wa Ujerumani Özil atangaza kustaafu soka

22 Machi 2023

Kiungo wa zamani wa Arsenal, Real Madrid na timu ya taifa ya Ujerumani Mesut Özil ametangaza kustaafu soka la kulipwa akiwa na umri wa miaka 34.

https://p.dw.com/p/4P4bU
Fußball WM 2010 Südafrika Deutschland gegen Serbien Flash-Galerie
Picha: AP

Özil ameshinda mataji tisa katika maisha yake ya soka ikiwemo taji la Ligi Kuu ya Uhispania La Liga mnamo mwaka 2012 na makombe manne ya Kombe la FA nchini Uingereza.

Aliichezea timu ya taifa ya Ujerumani Die Mannschaft mechi 92 na alikuwa sehemu ya kikosi kilichoshinda Kombe la Dunia la FIFA mwaka 2014 nchini Brazil. Akiwa na timu ya taifa ya Ujerumani, Özil alifunga mabao 23.

"Imekuwa safari ya kufurahisha iliyojaa wakati na hisia zisizosahaulika,” Özil ameandika katika taarifa yake kwenye mtandao wa kijamii.

"Nimekuwa na fursa ya kuwa mchezaji kwa karibu miaka 17 sasa na natoa shukrani za dhati kwa kupata nafasi hiyo.”

"Lakini katika wiki na miezi ya hivi karibuni, hasa baada ya kupata majeraha ya mara kwa mara, imekuwa wazi kwamba wakati wangu wa kuondoka uwanjani umefika.”

Ozil anajulikana kwa ujuzi wake wa kiufundi uwanjani, ubunifu, na alikuwa mchezaji mwenye kutoa pasi za uhakika.